Ujumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi ya Lesotho (IEC Lesotho) wamtembelea Waziri Mkuu Mst. Mhe. Pinda

Imewekwa: 27 Jul, 2022
Ujumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi ya Lesotho (IEC Lesotho) wamtembelea Waziri Mkuu Mst. Mhe. Pinda

Ujumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi ya Lesotho (IEC Lesotho) umemtembelea Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Mizengo Pinda shambani kwake Zinje Jijini Dodoma na kujionea shughuli za kilimo na ufugaji zinazofanyika kwenye shamba hilo.

Ujumbe huo umeongozwa na Mjumbe wa Tume hiyo Dkt. Karabo Mokobocho Monlakoana akiwa na Afisa Rasilimali watu wa IEC, Thato Moeti na Meneja Msaidizi wa Fedha Azael Limpho Monese na uliambatana na mwenyeji wao ambaye ni Mjumbe wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Asina Omar.

 

Wakiwa shambani hapo wametembea maeneo mbalimbali ya shamba hilo ikiwemo mabwawa ya kufugia samaki, shamba la zabibu, miembe na mazao ya mbogamboga.

 

Dkt. Karabo alishukuru namna Kiongozi huyo Mstaafu alivyowapokea na kuwatembeza kwenye maeneo mbalimbali ya shamba lake.

 

Mbali na kumtembelea Waziri Mkuu Mstaafu Pinda, kiongozi huyo wa IEC Lesotho na ujumbe wake pia wametembelea mji wa Serikali (Mji wa Magufuli) na kuipongeza Serikali kwa namna ilivyojenga miundombinu katika mji huo.